Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Simiyu
(Simiyurrh)

HOSPITALI YA RUFAA YA MKOA WA SIMIYU YAFANYA KIKAO CHA FUNGA MWAKA

Posted on: January 1st, 2020

Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Simiyu imefanya kikao cha watumishi wote siku ya tarehe 31/12/2019 ambapo katika kikao hicho Mwenyekiti alikuwa ni Mganga Mfawidhi wa Hospitali, Dkt Matoke Muyenjwa.

Dkt Muyenjwa alianza kwa kuwaomba watumishi wote wa Hospitali kuwa wasahameane sehemu yoyote waliyokwazana katika kutekeleza majukumu yao ya kitumishi. Pia aliwaomba watumishi wote  wazidi kupendana na kuendelea kuchapa kazi kwa juhudi na maarifa kwa mwaka 2020.

Picha: Watumishi wakiwa katika kikao cha mwisho wa mwaka  

Dkt Matoke alimkaribisha Mhasibu wa Hospitali Bw Shujaa Dennis Mkumbi ambaye alisoma mapato na matumizi ya Hospitali katika kipindi cha robo mbili za mwaka toka julai hadi desemba kwa mwaka wa fedha 2019/2020

Kaimu katibu wa Hospitali Bw Raphael Kambona aliwasilisha shughuli za Hospitali zilizofanywa katika kipindi cha miezi sita toka julai hadi desemba  2019. Bwana kambona alisema kuwa  katika kipindi hicho Hospitali imefanikiwa kufanya huduma za kliniki tembezi ambapo zaidi ya wateja 12250 walihudumiwa, upatikanaji wa dawa na vifaa tiba katika Hospitali ni zaidi ya asilimia 82, mazingira ya Hospitali yameboreka ikiwa ni pamoja na kupanda miti ya vivuli na matunda. Aidha miradi mikubwa ya ujenzi wa jengo la Radiolojia na upasuaji mkubwa, Maabara na kichomea taka yenye thamani ya jumla ya Tsh Bilioni 3.5 imetekelezwa. Kwa sasa Hospitali inaendelea na ujenzi wa jengo la Maama na mtoto la thamani ya Tsh Bilioni 5.7 na ujenzi  huo unatalajiwa kukamilika Septemba 2020.

Bwana kambona aliendelea kwa kusema kuwa rushwa kwa watumishi imepungua kwa zaidi ya asilimia 90. Hospitali imeendelea kukusanya mapato yake kwa kutumia mifumo ya GoTHOMIS na GePG  ambayo imerahisisha namna ya ukusanyaji fedha toka kwa wateja wa malipo ya papo kwa hapo  

Mwisho Dkt Matoke alihitimisha kikao hicho kwa kutoa vyeti kwa idara mbili zilizofanya vizuri katika utoaji wa huduma ambazo ni wodi ya watoto na idara ya magonjwa ya dharura

Picha: Mkuu wa kitengo cha magonjwa ya Dharura akionesha cheti cha ufanisi alichopokea

Kikao hicho kilimalizika kwa watumishi wote kupata chakula cha pamoja

Picha: watumishi wakipata chakula baada ya kikao